LORI LAPINDUKA NA KUUA WAFANYABIASHARA 6 NA KUJERUHI 12

Wafanyabiashara sita wamekufa papo hapo na wengine 12 kujeruhiwa, baada ya lori lililokuwa likiwapeleka mnadani kuacha njia na kuporomoka kwenye mlima wenye kona nyingi zinazofikia 99 wilayaniLushoto. 

Taarifa zilizopatikana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Benedict Wakulyamba zilisema ajali hiyo ilitokea jana Jumapili jioni katika mlima wenye idadi hizo za kona zinazoanzia Mng’aro hadi Mlalo wilayani Lushoto, baada ya lori aina ya Mitsubishi Fuso Canter kuporomoka. 

Watu walioshuhudia ajali hiyo walisema lori hilo lilikuwa likitokea Kijiji cha Mng’aro kilichopo uwanda wa chini lilipokuwa likipanda mlima kuelekea Mlalo kwa ajili ya kuwahi soko siku inayofuata. 

Walisema lori hilo lilipofika katikati ya mlima liliacha njia na kurudi nyuma hatimaye likaporomoka bondeni, huku mizigo ikiwaangukia watu hao. 

Kamanda Wakulyamba aliwataja waliokufa kuwa ni Jamal Hemed (40), mkazi wa Mlalo, Hassan Rashid (33) wa Nyasa, Bisura Seif wa Kifungilo, Hadija Said wa Mhelo, Zuena Juma wa Kwedege na Husna Athumani wa Hemtoye. 

Alisema majeruhi wa ajali hiyo walipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto kwa matibabu. Kamanda huyo alisema dereva wa lori hilo, Nassoro Athumani (25) anatafutwa kwa kuwa alitoroka baada ya ajali. 

Alisema uchunguzi wa awali unaonyesha chanzo cha ajali ni uzembe wa dereva na ubovu wa gari. 



Comments

Popular posts from this blog

ZINGATIA HAYA UKITAKA KURUDIANA NA MPENZI WAKO WA ZAMANI

ALAMA YA NYOKA KWENYE NEMBO MBALIMBALI INA MAANA KUBWA

Waziri Mkuu Ashangazwa Na Kodi Kubwa Soko La Dodoma.....Aagiza Baraza La Madiwani Lipitie Upya Na Kumpa Majibu